Monday, November 30, 2015

UKAWA KUCHUKUA JIJI LA DAR

Wafuasi wa vyama vinaonyounda Ukawa. 
Kama wingi wa madiwani katika halmashauri ndicho kigezo cha chama kumpata meya, basi safari hii jiji la Dar es Salaam litakuwa chini ya mameya kutoka vyama vinavyounda Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa).
Manispaa ya Ilala ambayo kuna karibu ofisi zote za Serikali zikiwamo wizara na Ikulu itakuwa chini ya meya wa Ukawa kwa mara ya kwanza kama ilivyo Kinondoni ambako karibu vigogo wengi wa serikali wanaishi.
Kwa mujibu wa matokeo ya uchaguzi wa madiwani katika jiji hilo, Manispaa ya Ilala ina jumla ya madiwani 52 wakiwamo wabunge watatu wa Ukonga, Segerea na Ilala. Kati ya madiwani hao CCM ina madiwani 22, Chadema 23 na CUF saba.
Ukawa inaundwa na vyama vya Chadema, CUF, NCCR-Mageuzi na NLD ambavyo vimeshatoa msimamo wa kusimamisha mgombea mmoja kwenye manispaa hiyo kuwania umeya.
Hii ina maana kwamba Chadema na CUF wakiungana, watakuwa na jumla ya madiwani 30 huku CCM ikiwa na 22.
Katika Manispaa ya Kinondoni, matokeo yanaonyesha kuwa kuna jumla ya madiwani 47 ambao wakichanganywa na wabunge wa majimbo ya Kawe, Kinondoni, Ubungo na Kibamba wanafika 51.
Mchanganuo wa vyama na idadi ya madiwani kwenye mabano ni CCM (15), Chadema (28) na CUF (8).
Katika mchanganuo huo, vyama vya CUF na Chadema vikiungana katika umoja wao vitakuwa na madiwani 36 ambao watapambana na wenzao 15 wa CCM, hivyo kuweka manispaa hiyo yenye idadi kubwa ya vigogo wa Serikali mikononi mwa Ukawa.
Kwa upande wa Manispaa ya Temeke ambayo ndiyo pekee CCM ina madiwani wengi Dar es Salaam, wapo 46 wakiwamo wabunge watatu wa Temeke, Mbagala na Kigamboni.

Kati ya madiwani hao, CCM ina 29 wakati Ukawa ikiwa na jumla ya madiwani 17, Chadema (9) na CUF (8).

0 comments:

Post a Comment

ZILIZOSOMWA ZAIDI