Tuesday, January 6, 2015

UKATILI DHIDI YA WANAWAKE: MWALIMU ALIYEPIGWA MARA NYINGI NA MUMEWE *PICHAZ*


Hali aliyokuwa nayo mwalimu Gaudencia Gitano baada ya kipigo cha mwaka 2012.Mwalimu Gaudencia Gitano (40) anayefundisha Shule ya Msingi Kivelu jijini Dar es Salaam, amedai huenda yeye ndiye anayeongoza kwa kupigwa kuliko wanawake wengine wote jijini, baada ya kudai anazo RB tano za vipigo tofauti kutoka kwa mumewe kwa nyakati mbalimbali tangu aolewe Oktoba 25, 2002, katika ndoa ya kiserikali iliyofungwa Ilala Boma.

Mwalimu Gaudencia Gitano (40) anayedai kupigwa mara nyingi na mume wake.
Akizungumza akiwa kitandani katika Hospitali ya Dar Group iliyopo barabara ya Nyerere jijini Dar es Salaam, Gaudensia (pichani), alidai kupigwa mara kwa mara kiasi kwamba katika vituo vya polisi na hospitali, amekuwa ni mwenyeji.
“Mimi ni mke wa pili kati ya watatu na tulifunga ndoa ya kiserikali na mume wangu Colman Marwa Oktoba 25, 2002 huko Ilala Boma. Tulikuwa tukipendana na Mungu ametujaalia tumepata watoto wawili, tulikuwa tukiishi pamoja katika nyumba yetu huko Kitunda na baadaye tukahamia katika nyumba yetu nyingine huko Msongola

Bi. Gaudencia Gitano akiuguza majeraha ya kipigo.
“Kipigo kilianza mara baada ya kuoa mke wa tatu, kukawa hakuna amani ndani ya nyumba, kila wakati ni kupigwa, nimechoka kutoa taarifa vituo mbalimbali vya polisi na kulazwa hospitalini, nimechoka na manyanyaso, ipo siku najua ataniua, Watanzania naombeni msaada wa kisheria kabla hajaniua.
“Huu ni mtiririko wa taarifa ya mashambulio ya kudhuru mwili nilizokuwa nikifungua katika vituo mbalimbali vya polisi, kwa mara ya kwanza aliponivunja mkono mwaka 2012 nilitoa taarifa katika kituo cha polisi Staki Shari jalada Na: STK/RB/10673/2012, kipigo cha pili nilifungua jalada Na: STK/RB/12631/2012, kilifuatia kipigo kingine nikafungua jalada No. KIT/RB/1400/2012, katika kituo cha polisi Kitunda.
“Vipigo havikuishia hapo, mwaka 2013, nilipigwa karibia kufa nikatoa taarifa polisi jalada Na. KIT/RB/2976/2013 na kipigo cha mwisho cha kufungia mwaka, hadi nilipopoteza fahamu nilifungua jalada Na. STK/ RB/ 17579/ 2014.
“Nakumbuka mwaka jana baada ya kuchoka na kipigo niliamua kuondoka na kupanga Kivule, alinifuata, akanipiga na kunivunja mkono, akachukua vitu vyangu vyote vya ndani, nilisononeka sana, nikanunua vingine, alirudi akanipiga na kuchukua tena vitu hivyo,” alisema mwalimu huyo kwa uchungu.

Mwalimu Gaudencia Gitano akiwa na mume wake.
Akisimulia zaidi, alisema licha ya vipigo hivyo, ambavyo anaamini siku yoyote vitamuua, lakini mwanaume wake huyo hawajali watoto kwa chochote, si chakula, matibabu wala mahitaji ya shuleni, ambapo kila kitu anakifanya mwenyewe.
“Mwaka 2012 nilifungua kesi katika Mahakama ya Mwanzo Ukonga nikihitaji talaka, aliandikiwa barua ya wito lakini hakufika katika kesi hiyo Na: 62, kwa hivi sasa nimechoka kwani nimekuwa nikifundisha nikiwa na manundu sehemu mbalimbali za mwili, wanafunzi wakiniuliza nashindwa cha kuwajibu, nawaombeni Watanzania mnisaidie kisheria, nimeshanusa kifo.
“Nitashukuru kwa watakaojitokeza kunisaidia, nawatakieni maisha mema, nawaomba mashemeji zangu endapo Mungu atanichukua kutokana na vipigo vya mara kwa mara, muwachukue watoto muwatunze, huyu hawezi kuwatunza.”
Mume wa mwalimu huyo, Colman Marwa alipopigiwa simu na waandishi wetu na kuulizwa kuhusu madai hayo alijibu kijeuri.
“Wewe kama unataka kumuwekea wakili muweke, huwezi kuniuliza mimi au nenda kawe wakili wake,” alisema na kukata simu.

0 comments:

Post a Comment

ZILIZOSOMWA ZAIDI