Sunday, August 24, 2014

SEHEMU YA BARABARA YA MANDELA JIJINI DAR KUFUNGWA KUANZIA TAR 25 HADI 30 AUGUST, 2014

MKANDARASI mkuu anaeshughulikia mradi wa mabasi yaendayo haraka jijini Dar es Salaam, Strabag International ametangaza kufungwa kwa muda kipande cha barabara ya Mandela hadi makutano ya Ubungo Mataa kuanzia leo.
Akiongea na waandishi wa habari, Ofisa Uhusiano wa kampuni hiyo, Bw. Yahya Mkumba alisema kipande cha barabara ya Mandela kuanzia makutano ya barabara ya morogoro upande wa kushoto uelekeo wa Tabata kuanzia ubungo mataa hadi darajani patafungwa.
Kipande hicho kitafungwa kuanzia tarehe 25/08/2014 mpaka tarehe 30/08/2014 ili kupisha ujenzi wa kipande cha barabara hiyo na hivyo kuwalazimu watumiaji wa barabara hiyo kutumia barabara ya upande mmoja.
Akifafanua zaidi ofisa uhusiano huyo alisema magari yatakayokuwa yanatokea Mwenge, Kimara na Shekilango yatalazimika kutumia barabara ya upande wa kulia ambayo pia itakuwa ikitumika na magari yanayo toka Tabata kuelekea Ubungo.
“Tunaomba radhi kwa usumbufu utakaotokea,” alisema Bw. Mkumba.
Mradi wa Mabasi yaendayo haraka unatarajiwa kuondoa adha ya foleni katika jiji hilo na kuleta ufanisi wa usafiri.
Awamu ya kwanza ya mradi huo inatarajiwa kumalizika mwishoni mwa mwaka huu.

0 comments:

Post a Comment

ZILIZOSOMWA ZAIDI