Sunday, September 27, 2015

MAALIM SEIF ASIKITISHWA NA AJIRA ZA WATOTO WILAYA YA MICHEWENI *PICHAZ*

 Mgombea Urais wa Zanzibar kwa tiketi ya CUF Mhe. Maalim Seif Sharif Hamad, akiangalia watoto wanaovyojihusisha na kazi ya uvunjaji wa kokoto katika Wilaya ya Micheweni, alipotembelea kikundi kinachojihusisha na kazi hiyo.
 Baadhi ya watoto wakijihusisha na kazi ya uvunjaji wa kokoto katika Wilaya ya Micheweni.
 Mgombea Urais wa Zanzibar kwa tiketi ya CUF Mhe. Maalim Seif Sharif Hamad, akiangalia kazi ya useremala inayofanywa na wananchi wa kijiji cha Wingwi na maeneo mengine ya Wilaya ya Micheweni.

 Mgombea Urais wa Zanzibar kwa tiketi ya CUF Mhe. Maalim Seif Sharif Hamad, akipandisha bendera ya chama hicho katika tawi jipya la CUF katika kijiji cha Kwale Micheweni, kuashiria ufunguzi rasmi wa tawi hilo.
Mgombea Urais wa Zanzibar kwa tiketi ya CUF Mhe. Maalim Seif Sharif Hamad, akipandisha bendera ya chama hicho katika tawi jipya la CUF katika kijiji cha Kwale Micheweni, kuashiria ufunguzi rasmi wa tawi hilo. (Picha na Salmin Said, OMKR)

Na: Hassan Hamad, OMKR
Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar Mhe. Maalim Seif Sharif Hamad, ameelezea kusikitishwa na ajira za watoto zinazoendelea katika Wilaya ya Micheweni.

Amesema ajira hizo hazifai na zinapaswa kupigwa vita kwa kulinda afya na ustawi wa watoto nchini.

Maalim Seif  ameeleza hayo wakati wa ziara yake ya kutembelea vikundi vya ujasiriamali katika Wilaya ya Micheweni ambapo amejionea shughuli mbali mbali zinazofanywa na wananchi wa Wilaya hiyo zikiwemo useremala, uvuvi, uchuuzi na uvunjaji wa kokoto.

Amesema watoto wengi katika wilaya hiyo wamekuwa wakijihusisha na uvunjaji wa kokoto pamoja na uvuvi na uparaji wa samaki, mambo ambayo yanakwenda kinyume na mikataba ya kimataifa.

Maalim Seif ambaye pia ni mgombea urais wa Zanzibar kupitia Chama Cha Wananchi CUF, amesema watoto wengi wanalazimika kujiingiza katika ajira hizo kutokana na uwezo mdogo wa wazazi wao, na kwamba iwapo atachaguliwa kuwa Rais wa Zanzibar atabadilisha maisha ya wananchi hao kwa kuweka mazingira ya kupata ajira zinazokubalika na zenye heshima.

Amesema serikali atakayoiongoza itaanzisha benki ya wajasiriamali, ili kutoa mikopo kwa wananchi kuweza kuongeza mitaji yao na kuendeleza vipaji vya wajasiriamali.

Amewashauri wajasiriamali wanaojihusisha na kazi ya useremala kuungana na kuunganisha nguvu zao ili waweze kuzifuata au kuagizia malighafi katika mikoa ya Tanzania bara, ili kuepusha ukataji miti ovyo katika visiwa vya Zanzibar, ambavyo vinakabiliwa na athari za mabadiliko ya tabia nchi yanayotokana na uchaguzi wa mazingira.

Katika risala ya wavunja kokoto iliyosomwa na ndugu Abdalla Omar Ali, wameomba kupatiwa mitaji na vitendea kazi vya kisasa ili kuondokana na usumbufu unaowakabili.

Nao wajasiriamali wa useremala wamesema wanakabiliwa na upungufu wa utaalamu, zana duni za kufanyia kazi, uchache wa malighafi pamoja na soko la kuuzia bidhaa zao, na kuomba kutafutiwa ufumbuzi wa matatizo hayo.

Hata hivo wamesema wamenufaika na kazi wanazozifanya ambazo zimeweza kuajiri zaidi ya watu mia tatu na kufanya zaidi ya watu elfu tatu kunufaika na ajira hizo.

Wakati huo Maalim Seif ambaye pia Katibu Mkuu wa CUF na mgombea urais wa Zanzibar, amefungua tawi la CUF katika kijiji cha Kwale Micheweni, na kuwataka wananchi kuacha kulumbana na tofauti za kisiasa.

Amesema Wazanzibari wanapaswa kuungana kutokana na Uzanzibari wao, na kuachana kulumbana kwa mambo ambayo hayatowaletea tija isipokuwa kuvuruga umoja na maridhiano ambayo yaliasisiwa kwa nia njema.

0 comments:

Post a Comment

ZILIZOSOMWA ZAIDI