Sunday, October 19, 2014

MAJERUHI WA AJALI YA MOTO WA LORI LA MAFUTA MBAGALA, HALI ZAO BADO NI MBAYA

MAJERUHI wa moto uliotokana na mlipuko wa lori la mafuta huko Mbagala Rangi Tatu jijini Dar es Salaam, waliolazwa katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili hali zao zinaendelea kuwa mbaya.
Juzi majeruhi wawili walifariki dunia baada ya ajali ya lori mali ya Kampuni ya Moil Transporter lililokuwa likisafirisha mafuta ya petroli kwenda Kampala, Uganda kupinduka likiwa na lita 38,000 za mafuta hayo yenye thamani ya Dola 36,000 za Marekani.
Ofisa Habari Msaidizi wa Hospitali ya Taifa, Muhimbili, Dorice Ishenda alisema jana, wagonjwa waliobakia hospitali wameendelea kubakia katika hali ilele na kwamba wawili kati yao hali zao zinaendelea kuwa mbaya.
Waliofariki dunia hadi kufikia juzi asubuhi ni Nurdin Mazinga (24) na Abbas Uganga (21), hivyo kufanya idadi yao kufikia sita na majeruhi wengine tisa wakiendelea kupata matibabu katika Hospitali ya Muhimbili.
“Hata hivyo, majeruhi saba wanaopata matibabu hali zao ni mbaya sana na wanahitaji uangalizi wa karibu zaidi. Madaktari wamekuwa wakiendelea kutafuta namna za kitaalamu zaidi kuwasaidia kutokana na majeraha makubwa ya moto waliyoyapata,” alisema.
Alisema kwamba ni majeruhi wawili tu kati ya tisa ambao hali zao angalau zinatia matumaini kutokana na kuweza kuzungumza na kutokuwa na majeraha makubwa ya kutisha.
Majeruhi hao wamelazwa katika wodi namba 23 ya Sewahaji iliyopo Muhimbili wakiwa na majeraha makubwa ya moto katika sehemu kubwa ya miili yao.
Wengine waliopoteza maisha awali kuwa ni Mohamed Hassan (36), Hassan Ismail (19), Maulid Rajab (61) na Mohamed Ismail (21). Idadi hiyo inafanya watu waliofariki dunia kutokana na ajali hiyo kufiki saba, akiwamo wa kwanza aliyefariki kwenye tukio hilo kabla ya kufikishwa hospitali.
Chanzo cha ajali 
Chanzo cha ajali hiyo ni watu waliokuwa wakichota mafuta ya petroli yaliyomwagika baada ya lori hilo kupinduka.
Wachotaji hao walikuwa wakificha mafuta hayo kwenye nyumba za jirani na mlipuko huo ulipotokea, moto ulifuata mafuta hayo na kuleta madhara kwenye eneo hilo.
Juzi Mganga mkuu wa hospitali ya Temeke, Dk. Amani Malima alisema walikuwa wamebaki majeruhi wanne baada ya 15 kuhamishiwa Muhimbili.

0 comments:

Post a Comment

ZILIZOSOMWA ZAIDI