Sunday, September 27, 2015

MAGUFULI AWATAJA WANACCM WANAOMSALITI HUKU WAKIMSANIFU KUWA WANAMUUNGA MKONO

MGOMBEA Urais kupitia Chama cha Mapinduzi (CCM), Dk. John Magufuli, jana aligeuka mbogo baada ya kuamua kuwataja hadharani watu wanaohujumu kampeni zake kwa kujifanya mchana wako pamoja na usiku wakigeukia upande wa upinzani.

Akiwahutubia wananchi wa mkoani Shinyanga jana katika mkutano wake wa kampeni uliofanyika katika Uwanja wa CCM Kambarage, Dk. Magufuli, alisema kuna mamluki wanaokihujumu chama hicho katika kuelekea uchaguzi mkuu unaotarajiwa kufanyika Oktoba 25, mwaka huu.

Dk. Magufuli aliwataja hadharani baadhi ya makada hao ambao wamekuwa wakiipigia kampeni CCM mchana na usiku wakiwapigia wapinzani.

 “Kuna baadhi ya wana-CCM wanatujuhumu sana, wengine nawajua hata majina yao bahati nzuri huwa sisemi uongo bali ukweli, kuna huyu Gasper mchana tunakuwa naye CCM lakini usiku anaungana na wapinzani,” alisema.

Hata hivyo, kauli hiyo ya Dk. Magufuli ilipokelewa kwa mshangao na  baadhi ya wananchi na wanachama waliokusanyika uwanjani hapo, kwa kuwa baadhi ya makada hao walikuwa wameketi jukwaa kuu wakifuatila hotuba yake.

Mwandishi wa habari hizi alimshuhudia meneja kampeni wa mgombea huyo, Abdallah Bulembo, akimfuata Magufuli na kumnong’oneza ghafla Magufuli alibadilisha na kudai msaliti ni Gasper Anthony wala si Gasper Kileo aliyetajwa awali.

Hata hivyo, Magufuli  baada ya kumaliza hotuba yake alimfuata kada huyo na kumkumbatia huku akimtuliza na kuendelea na msafara wake.

Kada huyo aliyetajwa kuwa msaliti anadaiwa awali kuwa mpambe wa mgombea wa urais kupitia Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Edward Lowassa, anayeungwa mkono na vyama vinavyunda Umoja wa Katiba (Ukawa).

Akizungumza katika mkutano huo wa kampeni, Kileo alisema alimuunga mkono Lowassa akiwa CCM, lakini kwa sasa anamuunga mkono mgombea urais wa chama hicho, Dk. Magufuli na wala kwa kilichotokea hatarajii kukihama chama.

Akiwahutubia mkoani Shinyanga, Magufuli amesema hashangai wananchi kuanza kumwita rais kwasababu hata yeye anajua kuwa ndiye atakayeibuka na ushindi mnono kwenye Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 25, mwaka huu.


Alisema wagombea wengine wa nafasi ya urais ni wasindikizaji tu kama walivyo wapambe wa kwenye harusi.

0 comments:

Post a Comment

ZILIZOSOMWA ZAIDI