Tuesday, April 29, 2014

WAPINZANI WATOA SABABU ZA KUSUSA NA KUTOSHIRIKI SHEREHE ZA MIAKA 50 YA MUUNGANO WA TANGANYIKA NA ZANZIBAR

BAADHI ya viongozi wa vyama vya upinzani wametoa sababu zilizowafanya wasihudhurie sherehe za maadhimisho ya miaka 50 ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar. 
Katika sherehe hizo zilizofanyika Jumamosi katika Uwanja wa Uhuru, viongozi wa vyama vikuu vya upinzani, Chadema, CUF na NCCR-Mageuzi hawakuonekana.
Katibu Mkuu wa Chadema, Dk Willibrod Slaa alisema kutokuonekana kwao hakuna uhusiano na msimamo wa chama wala Ukawa kama inavyodhaniwa.
“Mwenyekiti wangu (Freeman Mbowe), alikuwa safarini na kazi zake zote nazifanya mimi. Hata kama angekwenda uwanjani mimi nisingekwenda kabisa,” alisema.
Alisema alishaamua kutokwenda katika sherehe zozote za kitaifa kama maadhimisho ya Uhuru wa Tanganyika na Muungano tangu mwaka 2012 kutokana na sherehe hizo kugharimu fedha nyingi ambazo zingetumika katika maendeleo.
Alitaja sababu nyingine kuwa ni kuhusishwa na masuala ya kisiasa hususan chama tawala cha CCM.
Naibu Mkurugenzi wa Haki za Binadamu, Habari na Uenezi (CUF), Abdul Kambaya alisema chama chake kiliamua viongozi wote kutokuhudhuria sherehe hizo kutokana na kukosekana kwa maridhiano ya kujadili Rasimu ya Katiba inayozungumzia muundo wa Muungano.
Alisema chama kiliona hakuna sababu ya viongozi wake kuhudhuria sherehe za Muungano ambao majadiliano juu ya muundo wake yameshindwa na wajumbe wa Bunge Maalumu wameng’ang’ania muundo wa serikali mbili ambao haumo kwenye Rasimu.
“Wananchi wangetushangaa tumetoka bungeni juzi tu hapa halafu tunahudhuria sherehe za Muungano wenye makovu,” alisema Kambaya.
Alisema hakuna kiongozi wa chama chake aliyehudhuria katika sherehe hizo zaidi ya Katibu Mkuu wake, Seif Sharif Hamad ambaye alikwenda kwa shughuli za kiserikali akiwa Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar.
Katibu Mkuu wa NCCR-Mageuzi, Mosena Nyambabe alisema viongozi wa chama chake hawakuhudhuria kutokana na sababu zao binafsi... “Hatukukaa kama chama wala Ukawa kujadili kwamba tusihudhurie sherehe hizo,” alisema
 Chanzo: Mwananchi

0 comments:

Post a Comment

ZILIZOSOMWA ZAIDI