Tuesday, August 25, 2015

SPIKA AKUTANA NA VIONGOZI WA JUMUIYA YA NCHI ZA ULAYA ( EU) HAPA NCHINI

 SPIKA  wa Baraza la Wawakilishi, Zanzibar  Mhe. Pandu Ameir Kificho akiwa katika mazungumzo na Viongozi wa  Jumuiya ya  nchi za Ulaya ( EU) hapo Baraza la Wawakilishi Chukwani
SPIKA  wa Baraza la Wawakilishi, Zanzibar  Mhe. Pandu Ameir Kificho akiwa katika picha ya pamoja na Viongozi wa  Jumuiya ya  nchi za Ulaya ( EU) hapo Baraza la Wawakilishi Chukwani

Na, Himid Choko BLW. 

SPIKA  wa Baraza la Wawakilishi, Zanzibar  Mhe. Pandu Ameir Kificho  ameelezea matumaini yake kwamba  uchaguzi ujao utakuwa  huru na wa haki.

Amesema hali hiyo itachangia kwa kiasi kikubwa kuendelea  kuwepo kwa hali ya  amani na utulivu hapa nchini  suala ambalo ni muhimu kwa mustakbali  wa maendeleo ya taifa na ustawi wa jamii.

Spika Kificho amesema hayo leo, huko Afisini kwake  Chukwani wakati  akizungumza na Viongozi wa  Jumuiya ya  nchi za Ulaya ( EU)  waliongozwa na   Balozi wa Umoja  huo hapa  nchini  Bwa  Filiberto Sebregondi.

Kificho  ameufahamisha ujumbe huo kwamba,  ameridhishwa na ahadi zinazotolewa na wadau wote wa uchaguzi ikiwemo Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar (ZEC), Viongozi wa vyama vya Siasa na vyombo vya Ulinzi na Usalama kwamba kila kimoja kitatekeleza vyema wajibu wake  ili kufanikisha uchaguzi huo kwa njia ya haki, amani na usalama.


“Kila taasisi, tayari imetuhakikishia kwamba itatekeleza wajibu wake na kuondosha vikwazo vyote kwa lengo la kuendesha  salama mchakato wote wa Uchaguzi ambao tunaamini utakuwa wa haki na utulivu mkubwa” alisisitiza Spika Kificho.

Aidha spika Kificho ameuhakikishia umoja huo kwamba  Serikali zote mbili zitafanya kila liwezalo kuhakikisha kwamba hali ya amani  na usalama inaendelea kuwepo wakati na baada ya uchaguzi .

Kuhusu Serikali ya Umoja wa Kitaifa Spika kificho amesema mfumo huo ambao umekubaliwa na wananchi wenyewe upo kikatiba hivyo Baraza la Wawakilishi litafanya kila liwezavyo kulinda  matakwa  hayo ya wananchi.

Amesema chini ya mfumo wa Serikali ya Umoja wa Kitaifa ambao ni adimu duniani, maendeleo makubwa ya kisiasa na kiuchimi  yamepatikana  na umoja wa wananchi unazidi kuimarika  hapa Zanzibar.

Amesema  Baraza la Wawakilishi la Nane linalomaliza muda wake  lilikua la aina yake  ambapo chini ya mfumo wa Serikali ya Umoja wa Kitaifa Wajumbe wasiokua Mawaziri  waliibana vyema  serikali  kwa lengo la kuhimiza uwajibikaji , suala ambalo lilitoa mvuto mkubwa kwa wananchi kufuatilia   mikutano ya Baraza hilo.

Nae Balozi  Filiberto Sebregondi  amewaomba wadao wote wa uchaguzi kufuata sheria na taratibu zote  ili kufanikisha vyema  mchakato wote wa uchaguzi huru na wa haki.

Amesema jumuiya ya ulaya kwa kiasi kikubwa inafuatilia  mchakato huo  na kuwatakia kila la kheri  wananchi na hatimae waweze kufuka salama katika uchaguzi huu.
Mwisho.

Imetolewa na 
Himid  Choko
Afisi ya Baraza la Wawakilishi, Zanziabar,
25 August 2015

0 comments:

Post a Comment

ZILIZOSOMWA ZAIDI