Monday, April 14, 2014

LUKUVI: TUKIPITISHA SERIKALI TATU JESHI LITATAWALA NCHI

WAZIRI wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera Uratibu na Bunge), William Lukuvi ameanza kampeni kanisani kuwataka wananchi kupinga serikali tatu zilizopendekezwa na Tume ya Mabadiliko ya Katiba, vinginevyo nchi itatawaliwa na jeshi kwa kuwa Serikali ya Muungano itashindwa kuwalipa mishahara wanajeshi.
Alisema hayo jana katika Kanisa la Methodist, Jimbo la 
Dodoma alipokuwa mgeni rasmi akimwakilisha Waziri Mkuu, Mizengo Pinda.
Katika hotuba yake, Lukuvi aliwaeleza waumini waliofurika katika ibada ya kumsimika Mchungaji Joseph Bundala kuwa askofu wa kanisa hilo katika jimbo kuwa waendelee kuliombea Bunge lifanye uamuzi sahihi wa serikali mbili.
Aliwataka Watanzania kuipuuza Rasimu ya Katiba katika suala la Muungano na Serikali tatu kwa madai kuwa kutaka kuwapo mfumo huo ni kutaka Watanzania waingie vitani.
“Serikali tatu zikipita ni wazi kuwa hata makanisa yatafungwa kwani nchi haiwezi kuwa na amani tena, angalieni nchi ya Korea Kusini na Korea Kaskazini ambao waligawanyika na sasa ni maadui wakubwa wanaokaa mipakani wamenyoosheana bunduki,” alisema na kuongeza:
“Waumini ndugu zangu wapendwa, kwa sasa tupo katika hali mbaya sana hapo bungeni, tunaomba mtuombee kuna watu ambao wanataka madaraka kwa nguvu na wameanza kutafuta jinsi ya kuvunja Muungano na kudai kuwapo kwa Serikali tatu, nawaomba sana wapuuzeni wale wote ambao wanataka serikali tatu.”
Alisema watu wa aina hiyo wanaonekana kuwa wana huruma na Watanzania na wanadai kuwapo kwa Serikali ya Tanganyika wakati hiyo Tanganyika wanayoidai ni jina tu ambalo Wajerumani walikaa mezani wakabuni na kutuletea.
Lukuvi alisema Wazanzibari wanaotaka kuwa na nchi yao hawawezi kujitegemea, bali wanataka Serikali ili wapate nafasi ya kujitangaza kuwa ni nchi ya Kiislamu.
Alisema wanaopiga kelele wana ajenda za siri na nia yao kutaka kufanya fujo na kusababisha machafuko... “Kwani ukiwa na mke mmoja akakushinda unafikiri utatuzi ni kuoa mke mwingine?”
Baadaye alipotakiwa kufafanua kauli yake, Lukuvi alisema alichokizungumza kanisani hapo ni mawazo yake binafsi ambayo yanafanana na Watanzania wengi, akiwamo Rais Jakaya Kikwete.
“Unajua jeshi haliwezi kukaa na bunduki bila fedha. Hiyo Serikali ya tatu ambayo jeshi litakuwa chini yake haina vyanzo vya mapato vya kueleweka, sasa hao wanajeshi watalipwa nini? Wenye mitutu watakubali kuishi bila fedha?”
Alisema hata vyanzo vya mapato ambavyo vimeandikwa katika Rasimu ya Katiba ni lazima visimamiwe na pande mbili za Muungano, akiwa na maana ya Tanganyika na Zanzibar na kwamba kama upande mmoja ukishindwa kuchangia hali itakuwa mbaya.
“Kama tunataka serikali ya tatu ni lazima tuhakikishe kuwa inakuwa na vyanzo vya uhakika vya mapato. Jambo hili siyo ubishi wala ushindani ni suala la kujenga hoja na kujadili kwa kina, ni ngumu sana katika utekelezaji wake,” alisema.
Rais Kikwete wakati akizindua Bunge la Katiba mjini Dodoma aligusia suala hilo ambalo Lukuvi alilieleza katika ibada hiyo.
Kwa upande wake, Askofu Bundala alisema kanisani hapo kwamba ili kudumisha Muungano ni vyema Katiba ya Zanzibar ifutwe ili iwepo moja ya nchi moja ambayo inadumisha Muungano.
Alisema angetamani kumshauri Rais alivunje Bunge la Katiba kutokana na Bunge hilo kukosa mwelekeo na kukosa adabu.
Alipotakiwa kufafanua baadaye kuhusu kauli ya Lukuvi, askofu huyo alisema kuwa Waziri huyo hakutakiwa kutoa kauli nyepesi kama ile ukizingatia yeye ni mtu aliyepo madarakani.
“Kauli ya Lukuvi ilikuwa nyepesi sana kuzungumzia kwamba nchi itaingia kwenye vita. Ilitakiwa aende mbele zaidi kama mtu mwenye madaraka kwa kufafanua zaidi,” alisema.
“Mimi nataka serikali mbili kwa sababu tumeshazoea kusali chini ya miti tukiwa na amani na tukiwa na serikali tatu tutasali kwa mtutu. Kama umeshindwa kuwatunza wanawake wawili ulionao je, huyo wa tatu ambaye humjui tabia yake utamtunzaje?” alisema.

0 comments:

Post a Comment

ZILIZOSOMWA ZAIDI