Wednesday, March 19, 2014

AZAM YATOKA SARE NA YANGA LEO


BAO la dakika ya 83 la kinda Kevin Friday limeinusuru Azam FC kulala mbele ya Yanga SC baada ya kulazimisha sare ya kufungana 1-1 katika mchezo wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara.


Azam ilicheza kwa zaidi ya dakika 20 za mwisho ikiwa pungufu baada ya beki wake wa kulia, Erasto Nyoni kutolewa nje kwa kadi nyekundu kwa kutoa lugha chafu kwa refa. 

Mkombozi; Kinda Kevin Friday kushoto akishangilia na Gadiel Michael baada ya kufungia bao la kusawazisha Azam leo Uwanja wa Taifa
Ndiye mimi; Kevin Friday kulia akishangilia bao lake la ukombozi

Katika mchezo huo uliochezeshwa na refa askari wa jeshi la Polisi Tanzania, Hashim Abdallah wa Dar es Salaam aliyesaidiwa na Anold Bugado wa Singida na Florentina Zablon wa Dodoma, hadi mapumziko tayari Yanga walikuwa mbele kwa bao 1-0.


Bao hilo lilifungwa na mshambuliaji kutoka Burundi, Didier Kavumbangu dakika ya 14 aliyekutana na mpira uliorudi baada ya kupanguliwa na kipa Aishi Salum Manula kufuatia kutokea piga nikupige langoni mwa Azam. 

Shambulizi lililozaa bao hilo lilianzia kwa kwa Simon Msuva aliyemtoka beki Gadiel Michael wingi ya kulia na kutia krosi iliyounganishwa na Kavumbangu lakini mpira ukagonga mwamba na kurudi uwanjani na kumkuta Hamisi Kiiza aliyepiga kipa akaokoa na kumkuta mfungaji aliyemaliza kazi.

Azam FC ilikosa mabao mawili ya wazi kipindi cha kwanza, wakati bao lililofungwa na Kipre Herman Tchetche refa Hashim alikataa kwa sababu mpigaji kabla ya kufumua shuti alimsukuma beki Kevin Yondan.  

Wazee wa sebene; Didier Kavumbangu wa pili kulia akishangilia na wenzake baada ya kuifungia Yanga SC bao la kuongoza.

Wachezaji wa Azam mara mbili walimfuata refa Hashim kumlalamikia kwa kutoridhishwa na uamuzi wake, mfano alipokataa bao na mara moja alipokataa kutoa mpira wa adhabu baada ya John Bocco kuangushwa karibu na eneo la hatari.


Kipindi cha pili timu zote ziliingia na vikosi vile vile, Azam wakiendelea kusaka bao la kusawazisha na Yanga wakitaka kunenepesha ushindi wao.

Hata hivyo, nyota ya Yanga SC iliendelea kung’ara baada ya kupata penalti dakika ya 69 kufuatia beki Said Mourad ‘Mweda’ kuunawa mpira uliopigwa na Didier Kavumbangu, hata hivyo mkwaju wa Hamisi Kiiza ‘Diego’ ulipanguliwa vizuri na kipa Aishi Salum Manula na kuwa kona ambayo haikuzaa matunda. 

Baada ya kona hiyo wachezaji wa Azam wa Azam FC walikwenda kumlalamikia refa ambaye alimuonyesha kadi ya pili ya njano Erasto Nyoni na kuwa nyekundu.

Pamoja na kubaki wachache, Azam waliendelea na jitihada za kusaka bao la kusawazisha na dakika ya 83 kinda aliyepandishwa kutoka kikosi cha pili, Kevin Friday aliipokea vyema pasi ya Salum Abubakr ‘Sure Boy’ na kumchambua kipa mkongwe Juma Kaseja.

Kutoka hapo Azam walicharuka zaidi na kufanya mashambulizi mawili zaidi, lakini hawakufanikiwa kupata bao.

Kwa ujumla mchezo ulikuwa mkali na wa ushindani- wenye hadhi ya Ligi Kuu kweli. Azam FC sasa inajiongezea pointi moja na kufikisha pointi 44 baada ya mechi 20, wakati Yanga SC inatimiza pointi 40 baada ya mechi 19.
  
Kikosi cha Yanga SC kilikuwa; Juma Kaseja, Juma Abdul, Oscar Joshua, Nadir Haroub ‘Cannavaro’, Kevin Yondan, Frank Domayo, Simon Msuva, Hassan Dilunga, Didier Kavumbangu/Mrisho Ngassa dk73, Hamisi Kiiza/Hussein Javu dk87 na Emmanuel Okwi.

Azam FC; Aishi Manula, Erasto Nyoni, Gadiel Michael, Said Mourad, Kipre Balou, Himid Mao, Salum Abubakar, John Bocco, Kipre Tchetche na Khamis Mcha/Kevin Friday dk49.

Kwa hisani ya Bin Zubeiry blog

0 comments:

Post a Comment

ZILIZOSOMWA ZAIDI