Monday, August 17, 2015

TUME YA UCHAGUZI ‘NEC’ YAOMBWA ZOEZI LA UPIGAJI KURA LIANZE SAA 12:00 ASUBUHI SHINYANGA

DSC01147
Baadhi ya waandishi wa habari 25 kutoka mikoa ya Singida, Katavi, Kigoma na Shinyanga,waliohudhuria mafunzo ya uandishi bora wa habari za uchaguzi yaliyofanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa Vigimark hotel nje kidogo ya mji wa Shinyanga. Mafunzo hayo ya siku tano, yaliratibiwa na Baraza la habari (MCT) na kufadhiliwa na BBC Media Action .Wa tatu kulia waliosimama, ni mwandishi wa habari wa Modewji blog, Singida, Bw. Nathaniel Limu.
Na Nathaniel Limu, Shinyanga
AFISA uchaguzi manispaa ya Shinyanga, Joseph Sengerema, ameiomba tume ya uchaguzi (NEC) kuangalia uwezekano wa zoezi la upigaji kura kuanza saa 12.00 asubuhi, ili kuondoa uwezekano wa kura kuhesabiwa kwa msaada wa mwanga wa taa ya simu ya kiganjani.
Sengerema ametoa rai hiyo wakati akitoa taarifa ya mafanikio ya zoezi la kuhakiki wa wapiga kura kwenye daftari la kudumu la wapiga kura, kwa waandishi wa habari waliomtembelea ofisini kwake.
Alisema uzoefu unaonyesha kuwa kumetokea baadhi ya vituo vya kupigia kura kuhesabu kura hadi nyakati  za usiku na vingi vipo maeneo ya vijijini ambavyo havina huduma ya umeme.
Akifafanua, Sengerema alisema kuhesabu kura nyakati za usiku licha ya kuwa ni hatari kwa maisha ya maafisa wanaohesabu kura, pia husababisha hofu ya kuibiwa kwa kura na kupelekea kufanyika vitendo vya uvunjivu wa amani na utulivu sehemu husika.
“Umefika wakati sasa tume ya uchaguzi kuangalia upya zoezi la upigaji kura, kuanza mapema zaidi ili uhesabuji kura uweze kufanyika mchana kweupe kabla ya kuingia kwa giza”,alifafanua zaidi afisa huyo.
Katika hatua nyingine, Sengerema amewataka wapiga kura kujenga utamaduni wa kuhakiki kumbukumbu zao kwenye daftari la kudumu la wapiga kura kupitia simu zao za viganjani.
“Zoezi la kuhakiki kumbukumbu kwenye daftari la kudumu la wapiga kura kupitia simu za viganjani ni endelevu.Kumbukumbu hizo zinapatikana kwa kubofya *152*00# kisha kujaza namba ya mhusika ya kadi/kitambulisho  cha kupigia kura”,alisema.
Kwea mujibu wa afisa huyo,manispaa ya Shinyanga,imefanikiwa kuvuka lengo la kuandikisha wapira kura kwenye daftari la kudumu,kwa asilimia 101 dhidi ya lengo la kuandikisha wapiga kura 98,000 kwenye vituo 158.
#Modewji blog

0 comments:

Post a Comment

ZILIZOSOMWA ZAIDI