Sunday, January 4, 2015

TAHARUKI YA PANYA ROAD YAIBUA MAPYA, DIAMOND NAYE ALIKUWA PANYA ROAD *PICHA*

Ayubu Mohamed maarufu Diamond enzi za uhai wake.
*****
Na Ibrahim Yamola na Kalunde Jamal, Dar es Salaam.
BAADA ya saa 24 kupita tangu kundi maarufu la waporaji la Panya Road, kuvamia na kusababisha shughuli mbalimbali kusimama kwa wakazi wa Jiji la Dar es Salaam, chanzo cha uhalifu huo kimebainika.
Hali hiyo iliwafanya wakazi wa jiji hilo kusitisha shughuli mbalimbali kutokana na kuhofia usalama wao, huku usafiri ukiadimika.
Tukio hilo linaelezwa lilitokea ikiwa ni ishara ya kundi hilo kumuenzi mwenzao aliyefikwa na mauti akidaiwa kutaka kuiba pikipiki.
Mkazi wa Magomeni Kagera, Mohamed Chalamira alisema, “Wakati wakitoka kuzika walikuwa wakiambiana kuwa mwanajeshi hawezi kuuawa na kuzikwa bila kupigwa mizinga hivyo tutakwenda kulianzisha ili polisi wapige mabomu na ndicho kilichotokea.”
Aliongeza: “Ni tukio lililotuacha tukishangaa, kwani polisi mmoja aliyekuwa na silaha alitaka kumkamata mwenzao, lakini alipotoa panga tu yule polisi alikimbia, hii haiwezekani yaani polisi anakimbia mhalifu? Ilikuwa saa 9 vijana waligeuza eneo hilo (Magomeni Kagera) kama eneo lao.”
Kuhusu vijana waliokamatwa Chalamira alisema: “Hao vijana wawili waliokamatwa mmoja kweli anahusika, lakini mwingine ni hahusiki kwani dereva, huyo mshikaji atasota huko wakati hahusiki, polisi wafanye uchunguzi wao kwani haiwezekani kundi hili likasababisha mtafaruku...Mimi mwenyewe juzi nimepoteza simu na nimeumia hapa katika goti.”

Familia yazungumza
Kaka mkubwa wa marehemu, Mohamed Ayubu maarufu ‘Diamond’, Moshi Hamadi alisema mdogo wake huyo alizaliwa mwaka 1995 Magomeni Kagera na kukulia kwenye familia hiyo, lakini aliondoka kutokana na tabia zake kuanzia kubadilika.
Alisema Ayubu hakubahatika kumaliza elimu ya msingi kutokana na kujiingiza katika makundi ya wavuta bangi akiwa darasa la nne na alipoonywa hakukubali na alichukia na kuamua kuondoka nyumbani kwao.
“Huyu alikuwa ni mtoto wa pekee kwa mama yake, hakuwahi kupata mtoto mwingine, ndiyo maana hawezi kuzungumza presha imempanda,” alisema Hamad baada ya mwandishi kuomba kuzungumza na mama yake mzazi na alijibiwa hivyo.
Kauli ya Hamadi iliungwa mkono na mama mkubwa wa marehemu Ndam Moshi ambaye alisema Ayubu hakutaka vitendo vyake vijulikane na alipokuwa akienda kuwasalimia walipomgusia kwamba siku hizi anajihusisha na masuala ya wizi alikuwa anakataa na kulia kutwa nzima.
Kuhusu taarifa za kifo chake, Hamadi alisema walipigiwa simu na vijana wasiowafahamu kuwataarifu kuwa Diamond amefariki dunia kwa kukatwa mapanga eneo la Tandale kwa Mtogole ambako kulikuwa na mkesha wa Mwaka Mpya.
Mkazi wa Tandale karibu na eneo walipouona mwili wa Ayubu ambaye hakutaka kutajwa jina lake alisema: “Tuliamka asubuhi juzi (Januari Mosi) na kuambiwa kuna mwili umetupwa pale darajani (Daraja la Kwa Sindano linalotenganisha Tandale na Sinza-Yemen).”
Aliongeza: “Hapo ilikuwa kama saa tatu asubuhi, tuliukuta mwili wa kijana huyo ukiwa uchi wa mnyama huku tofali kubwa likiwa limewekwa kichwani kwake...Polisi walikuja na kuondoka nao mwili wa marehemu hatukujua walipokwenda kuuhifadhi.”
Hamadi alisema mwili wa marehemu waliukuta katika Hospitali ya Taifa Muhimbili ukiwa umekatwa kwa mapanga maeneo ya kichwa na kuufanya kuharibika na miguu ikiwa kama imechomwa moto na ukiwa hauna nguo.
Mama mkubwa wa marehemu Ndam alisema kuwa hajawahi kukaa msibani kwa wasiwasi kama msiba huo, alisema kilichokuwa kinatokea nje katika msiba huo kilitaka kusababisha mauti ya mama yake Ayubu kutokana na presha, kwani kulikuwa na idadi kubwa ya vijana ambao hakuwafahamu.

Kwa nini msiba huo umehusishwa na Panya Road?
Hamadi alisema walipokuwa wanarudi na mwili wa marehemu kutoka Muhimbili walikuta kundi kubwa la wahuni limetanda maeneo ya jirani na nyumbani kwao na kadiri walivyokuwa wakisogea ndiyo walizidi kukuta umati wa wahuni.
Alifafanua hakuwa akimfahamu hata kijana mmoja kati yao wala ndugu zake hakuna aliyekuwa akiwafahamu kila mtu kwenye familia hiyo alikuwa anashangaa.
“Baada ya kufika waliupeleka mwili wa marehemu moja kwa moja Msikiti wa Magomeni Kagera uitwao Masjid Rahman kwa ajili ya kuswalia, kwani kila kitu kuosha na kuuandaa mwili wa marehemu kwa ajili ya mazishi ilifanyika Muhimbili,” alisema Hamadi.

Hali ilikuwaje msikitini hadi makaburini
Tofauti na kauli zilizokuwa zikitolewa na wengi kuwa maziko ya kijana huyo yalitawaliwa na vitendo vya kihuni, Shekhe Hassan Khamisi Majaliwa ambaye ni babu wa marehemu na ndiye aliyeongoza mazishi ya kijana Ayubu alisema hakukuwa na vurugu hadi walipomaliza kuzika.
“Baada ya kupokea mwili uliswaliwa kabla ya swala ya saa kumi na baada ya kuuswalia na kutoka nje ndipo vijana hao ambao kwa miaka 40 niliyoishi hapa sikuwahi kuona umati wa vijana kama hao...Vijana hao waliupokea mwili na kuubeba wenyewe kistaarabu na kumkataza mtu yeyote kushika jeneza kwa madai kuwa hawamfahamu kama wanavyomfahamu wao.”
“Walipofika katika makaburi ya Kihata (nyuma ya msikiti huo) aliwataka watulie na wao kwa wao wakawa wanatulizana isipokuwa mmoja wao alikuwa kalewa na alishika betri ya simu alikuwa akifanya kama vile anachukua picha, baada ya kisomo wakati mwili unafukiwa akalirusha hilo betri likafukiwa na udongo hicho ndiyo kitu pekee kilichowekwa ndani ya kaburi hilo,” alisema Sheikh Majaliwa.
Alisema baada ya mazishi kumalizika aliwataka vijana wasifanyie fujo za aina yoyote katika eneo hilo kwa sababu lawama itakua kwao.
“Walikubali, lakini nilikuwa nasema kujifurahisha, kwani sura zao zilivyokuwa nilifahamu lazima watafanya fujo na kweli walifanya hivyo,” alisema.
Aliongeza: “Tulipokuwa tunatoka makaburini saa 11.45 jioni tuliwakuta polisi wametanda maeneo haya na walipoona kundi la watu waliwatawanya vijana hao kwa kufyatua risasi.”

Mashuhuda wazungumzia
Vijana waliokuwa kwenye kijiwe cha Magomeni Kagera ambao hawakuwa tayari kutaja majina yao waliliambia gazeti hili kuwa hali ilikuwa mbaya kwani kila mtu alikuwa anakimbia kunusuru roho yake.
Walisema Polisi wakiwa ndani ya gari waliloegesha eneo hilo kuna dada aliibiwa simu na hao Panya Road, lakini vijana wa eneo hilo wakawakimbiza na kuwanyang’anya simu na kumrudishia mwenyewe huku, Polisi wakitizama tukio hilo.
Vijana waliokuwa kijiwe eneo la Tandale kwa Mtogole walisema walikuwa wanamfahamu Ayubu wakati wa uhai wake, lakini hawakuwa wakijua kijiwe chake maalumu ni wapi kwa sababu alikuwa anafahamika kila kona.

Kaniki
Katika hatua nyingine makamanda wa polisi mkoa wa Dar es Salaam, akiwemo Kamanda wa Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Suleiman Kova, wametakiwa kutodharau taarifa za uhalifu zinazotolewa na wananchi kwa kisingizio cha madai ya uvumi.
Taarifa toka ndani ya Jeshi la zilizolifikia gazeti hili jana zilisema kuwa hayo yalielezwa na Naibu Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini, Abdulrahman Kaniki alipokutana na makamanda hao katika kikao cha dharura kilichofanyika Makao Makuu ya jeshi hilo.
Kwa mujibu wa taarifa hizo, Naibu IGP, alisisitiza kwa makamanda hao umuhimu wa kuthamini na kuzifanyia uchunguzi wa haraka taarifa za uhalifu zinazotolewa na wananchi.

Panya road 36 mbaroni
Kamanda wa Kanda Maalum ya Dar es Sala Seleima Kova alisema tangu tukio hilo lilipotokea wameendelea na msako mkali na kufanikiwa kuwatia nguvuni vijana 36.
“Tunawashikilia vijana 36 na msako huu unaendelea, tunawakamata wale wote wenye rekodi ya kufanya uhalifu...tunawaomba wananchi wanaotumia mitandao ya kijamii kuepuka kutuma taarifa ambazo hawana uhakika nazo ambazo kwa namna moja au nyingine zinahatarisha usalama,” alisema Kova
Baadaye, Taarifa kwa umma iliyotolewa na Msemaji wa Jeshi la Polisi nchini, Advera Bulimba alisema, “Jeshi la Polisi linatoa onyo kwa vijana hao wanaojihusisha na vikundi hivyo kuacha tabia hiyo mara moja. Tumejipanga vizuri katika mikoa yote kuhakikisha kwamba nchi inaongozwa kwa kufuata utawala wa sheria, hatutamwonea mtu yeyote ama kikundi cha watu wanaotaka kuvuruga amani ya nchi na kutia hofu wananchi.”
Kamanda wa Polisi wa Ilala, Mary Nzuki alisema kijana mmoja ameuwawa eneo la Kipunguni-Mombasa jijini Dar es Salaam saa 10 alfajiri ya kuamkia jana.

Chanzo: mwananchi.co.tz

0 comments:

Post a Comment

ZILIZOSOMWA ZAIDI