Wednesday, August 12, 2015

MTOTO WA ZARI AMLIZA MWANAMUZIKI DIAMOND PLATNUMZ


HII ni kali! Muda mchache baada ya mwandani wake, Zarinah Hassan ‘Zari The Boss Lady’ kujifungua salama, staa wa Bongo Fleva, Nasibu Abdul ‘Diamond Platnumz’, amejifungia chemba kisha kuangua kilio akisema Mungu ni mwema huku akiwataja waliowahi kuwa wapenzi wake, Penniel Mungilwa ‘Penny’ na Jokate Mwegelo kwa maneno yao ya shombo.

TUJIUNGE AGA KHAN
Tukio la kujifungua mchumba wa Diamond, Zari lilijiri Agosti 6, mwaka huu mishale ya saa 10:40 alfajiri katika Hospitali ya Aga Khan jijini Dar  ambapo alipelekwa usiku huo baada ya kujisikia uchungu ambapo alijifungua mtoto huyo wa kike.
Chanzo cha habari kilieleza kwamba, siku hiyo, wakiwa hospitalini hapo, muda mfupi tu baada ya Diamond kuambiwa kuwa tayari Zari amejifungua, jamaa huyo alilipuka kwa shangwe na baadaye akajifungia chemba na kuanza kulia.

Kilipenyeza kuwa baadhi ya watu walioshuhudia walijiuliza kisa cha kulia ambapo baadaye alisema kuwa watu walikuwa wamemsema mengi juu yake na ishu kupata mtoto.

AANGUA KILIO
“Diamond alijikuta akiangua kilio, suala ambalo mwenyewe lilianza kunitia hofu maana kabla hajaanza kulia alikuwa akichekelea na hatukujua aliingiwa na nini hadi akaanza kulia huku akimshukuru Mungu kwa kumletea mtoto.
“Ila nilipomuuliza zaidi kinachomliza alisema kuwa amejikuta akifurahia hadi kulia kwani kabla Zari hajajifungua, alikuwa akiwaza sana kutokana na maneno ya watu ambao wengine walikuwa wakimwandikia meseji na kumtishia kuwa hawezi kuzaa salama,” kilitiririka chanzo hicho na kuongeza:

“Eti alisema kwamba, kuna siku alikuwa hapati kabisa usingizi kufuatia ishu ya kutopata mtoto hasa anapowaza maneno ya watu na mara nyingine alipokuwa akikumbuka maneno ya Penny na Jokate ambao walikuwa wakisema hana kizazi hivyo Mungu alikuwa amewajibu bila kinyongo yote waliyokuwa wakimuombea mabaya.

HUYU HAPA DIAMOND
Baada ya kupenyezewa ‘ubuyu’ huo, gazeti hili lilimtafuta Diamond ili kumdadisi zaidi juu ya kilio hicho ambapo alipopatikana alisema kuwa anamshukuru sana Mungu kwa kutimiza ndoto yake na kwamba sasa milango ya heri imefunguliwa hivyo hana sababu ya kueleza machungu yote aliyokuwa nayo zaidi ya kumshukuru  Mungu kwa kuwa yeye ndiye mweza wa yote.
“Siwezi kuweka wazi hilo ila kikubwa ninachoweza kusema kwa sasa namshukuru Mungu kwa kunianzishia historia mpya hivyo namuomba aendelee kumlinda mke wangu na familia yangu,” alisema Diamond.

Hadi gazeti hili linakwenda mitamboni, bado Zari alikuwa hospitalini huku mama Diamond, Sanura Kassim ‘Sandra’ akimhudumia mtori huku mtoto huyo akipewa jina la Latifah a.k.a Princes Tifah au Queen Latifah.
#GPL

0 comments:

Post a Comment

ZILIZOSOMWA ZAIDI