Saturday, January 3, 2015

MWAKA WA UCHAGUZI: VITA DHIDI YA URAIS 2015, MITANDAONI KWACHAFUKA BALAA!!

WAKATI safari ya kuelekea kwenye Uchaguzi Mkuu wa Oktoba mwaka huu ikipamba moto, kumeibuka makundi ya watu yaliyofungia akaunti katika mitandao ya kijamii yakiwaunga mkono baadhi ya wanasiasa waliotangaza au wanaotajwa kuwa na nia ya kugombea urais ya kuwashambulia washindani wao.

Kila kundi limejipatia wafuasi wengi ambao wanaonyesha kumkubali mwanasiasa husika wanayedhani anafaa kuwa rais wa Tanzania endapo atapitishwa na chama chake na kupigiwa kura na wananchi.

Hata hivyo, wasomi na wachambuzi wanaonya kuwa pamoja na njia hii kuwa ya haraka kuwafikia wapigakura walio wengi ambao ni vijana na wanawake, inatakiwa kutumika kwa uangalifu la sivyo inaweza kusababisha machafuko.

Kurasa zinazotamba kwa sasa huko Facebook ni zile za Team lowassa, Team Hamis Kigwangalla, January Makamba – The next President’, Bernard Membe Fans Page, Dr Slaa Team Winner na Marafiki wa Samwel Sitta

Katika mtandao wa Twitter, wanasiasa hao na wengine hawako nyuma, karibu kila mmoja ana akaunti binafsi huku wafuasi wao wakipata nafasi ya kusoma yale wanayoyaandika wakati wowote.

Miongoni mwa wanasiasa wenye wafuasi wengi ni Zitto Kabwe ambaye watu 208,294 wanafuatilia hoja zake na wakati mwingine kujibizana.

Anayefuata ni Makamba mwenye wafuasi 151,822, Bernard Membe (45,889) na Dk Slaa (40,830). Lazaro Nyalandu aliyetangaza wiki iliyopita kuingia katika mbio za kusaka urais, akaunti yake ya Twitter inafuatiliwa na watu 36,726.

Wengine katika mkondo huo ni Dk Khamis Kigwangalla (26,322), William Ngeleja (11,110), Anna Tibaijuka (8,053), Freeman Mbowe (4,162), Asha-rose Migiro (4,736), Edward Lowassa (2,123), Stephen Wasira (750) na Dk Emmanuel Nchimbi (515).

Ni dhahiri kuwa wanasiasa vijana ndiyo wanaotumia zaidi mitandao ya kijamii na kuwa na wafuasi wengi ambao wengi wao pia ni vijana.

0 comments:

Post a Comment

ZILIZOSOMWA ZAIDI