Tuesday, May 27, 2014

CECAFA YAHUZUNISHWA NA KIFO CHA MTOTO MCHEZA MPIRA NA WAWILI KUJERUHIWA NCHINI SOMALIA

Katibu mkuu wa CECAFA, Nicholas Musonye akizungumza katika moja ya semina ya FIFA iliyofanyika jijini Dar es salaam hivi karibuni.
Na Baraka Mpenja, Dar es salaam
BARAZA la vyama vya soka ukanda wa Afrika mashariki na kati, CECAFA limeungana na nchi ya Somalia kuomboleza kifo cha mtoto mmoja mcheza mpira na wengine wawili kujeruhiwa kutokana na mlipuko wa bomu lililotegwa katika uwanja wa wazi mjini Balanbale karibu na mpaka wa Ethiopia.
Mwa mujibu wa taarifa iliyotumwa katika mtandao huu na Afisa habari wa chama cha soka nchini Somalia, Shafi’i Mohyaddin Abokar imesema ili kuungana na Somalia katika kipindi hiki kigumu baada ya tukio hilo la kuhuzunisha, katibu mkuu wa CECAFA Nicholas Musonye ametuma salamu za rambirambi kwa katibu mkuu wa chama cha soka nchini Somalia Abdi Qani Said na kutoa pole kwa taifa hilo changa katika maendeleo ya soka.
“Nimesoma habari za kuhuzunisha juu ya kifo cha mchezaji kijana na wawili kujeruhiwa wakati wakicheza mpira nchini Somalia. Naungana na wewe na familia ya mtoto aliyefariki katika kipindi hiki cha huzuni”. Alisema katibu wa CECAFA katika barua yake ya salamu za rambirambi kwa katibu mkuu wa chama cha Somalia jana jioni.
Bwana Musonye alisema CECAFA siku zote inaamini kuwa ipo siku itatokea Somalia yenye utulivu ambapo maendeleo ya mpira yatapatikana na wachezaji wake watajitangaza kimataifa.
“Tunaamini wachezaji wawili waliojeruhiwa wataendelea vizuri na tunawaomba wazazi wawe wavumilivu wakati huu wa huzuni” . Musonye aliendelea katika barua yake ya Salamu za rambirambi.

0 comments:

Post a Comment

ZILIZOSOMWA ZAIDI